• HABARI MPYA

    Monday, March 02, 2015

    SIMBA SC WAENDA ZENJI KUIANDALIA DOZI YANGA SC

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    KIKOSI cha Simba SC kimeondoka jana Dar es Salaam kwenda Zanzibar kuweka kambi ya kujiandaa na mchezo dhidi ya mahasimu wao wa jadi, Yanga SC Jumapili.
    Simba SC ambayo juzi iliihadharisha Yanga SC baada ya kuitandika Prisons mabao 5-0 Uwanja wa Taifa, imekwenda Zanzibar kwa ajii ya maandalizi mazuri kama ilivyo ada yake unapowadia mchezo huo.
    Zanzibar sasa ndiyo sehemu ambayo Simba SC wanaiamini zaidi kwa kambi za kujiandaa na mashindano mbalimbali na kuelekea mchezo wa Machi 8, 2015 wamerudi huko tena.
    Kocha wa Simba SC, Goran Kopunovic akiwa mwenye furaha juzi timu yake ikishinda 5-0

    Kocha Mserbia, Goran Kopunovic alikuwa mwenye furaha baada ya ushindi wa 5-0 dhidi ya Prisons Jumamosi Uwanja wa Taifa na akasema anaelekeza nguvu zake kwenye mchezo ujao.
    Wakati Nahodha Joseph Owino amerejea kikosini, Waganda wenzake, Juuko Murushid na Simon Sserunkuma wamerejea kwao Uganda kwa matatizo ya kifamilia.
    Lakini Simba SC inaonekana kuwa madhubuti hata bila ya Waganda hao wawili waliosajiliwa msimu huu.  
    Upande wa pili, Mkutano Mkuu wa wanachama Jumapili ya jana ulirejesha hali shwari klabuni, kufuatia kuwapo taarifa kwamba Rais wa klabu, Evans Aveva ‘haivi’ na Makamu wake, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’.
    Wawili hao wote walizungumza mbele ya wanachama wachache waliojitokeza mkutanoni kwamba hakuna tatizo baina yao na kuna mshikamano wa kutosha ndani ya uongozi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC WAENDA ZENJI KUIANDALIA DOZI YANGA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top