• HABARI MPYA

    Wednesday, March 25, 2015

    MSUVA AFIKISHA MABAO 29 KATIKA MECHI YA 93 YANGA SC, SASA NDIYE ‘BOSI WA MABAO LIGI KUU’

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    WINGA machachari, Simon Happygod Msuva leo amefikisha mabao 29 katika mwechi 93 alizoichezea Yanga SC kwenye mashindano yote tangu ajiunge na klabu hiyo mwaka 2012.
    Msuva amefunga mabao mawili leo, moja kila kipindi Yanga SC ikishinda 3-1 dhidi ya JKT Ruvu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara. 
    Aidha, Msuva pia amepanda hadi nafasi ya kwanza kutoka ya pili, katika mbio za ufungaji bora wa Ligi Kuu, kwa kufikisha mabao 11 msimu huu, akimzidi kwa bao moja, Mrundi Didier Kavumbangu wa Azam FC.
    Msuva alifunga bao lake la 10 katika Ligi Kuu msimu huu dakika ya 33 kwa mkwaju wa penalti na kumfikia Kavumbagu.
    Simon Msuva akishangilia baada ya kufunga bao lake la 29 leo Yanga SC katika mechi ya 93

    Penalti hiyo ilitolewa baada ya beki wa JKT Ruvu, Ramadhani Haruna Shamte kuunawa mpira uliopigwa na Msuva na refa Isihaka Shirikisho wa Tanga, aliyesaidiwa na Milambo Tshikungu na Mashaka Mandembwa, wote wa Mbeya ‘akatenga tuta’.
    Msuva, tena alimalizia pasi ya Ngassa kufunga bao la tatu dakika ya 57 na sasa mbio za ufungaji bora wa Ligi Kuu, ni yeye na Kavumbangu.
    Msuva pia ndiye aliyetoa pasi ya bao lingine la Yanga SC katika mchezo wa leo lililofungwa na Danny Mrwanda dakika ya 41. Huku kukiwa kuna tetesi kwamba, Mrisho Ngassa ataondoka Yanga SC mwishoni mwa msimu- basi hapana shaka, Msuva atakuwa mfalme mpya Jangwani.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MSUVA AFIKISHA MABAO 29 KATIKA MECHI YA 93 YANGA SC, SASA NDIYE ‘BOSI WA MABAO LIGI KUU’ Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top