• HABARI MPYA

    Saturday, December 20, 2014

    SIMBA NI WAKATI SASA WA KUIANZA SAFARI YA UJENZI WA UWANJA WENU

    Na Hemed Hamis, DAR ES SALAAM
    NAANZA kwa kuipongeza klabu ya Simba kwa ushindi ulioupata kwenye mechi ya mtani jembe. Hii ikiwa ni mara ya pili mfululizo. Kweli mwenye bahati habahatishi, siku tatu baadae hukumu yenu ya kesi dhidi ya club etoile du sahel imetoka na kuwapa ushindi utakaopelekea kuvuna si chini ya tsh 500mil. Mungu awepe nini?. Na hapa ndipo msingi wa mada yangu utakapojikita.
    Ni kwa muda wa miongo kadhaa kumekuwapo na hitajio la klabu ya simba kuwa na uwanja wake. Tangu enzi ya kuwa na sehemu ya mazoezi katika moja ya viwanja vya wazi eneo la jangwani, jirani na yalipo makao makuu ya klabu ya yanga.japokuwa viwanja hivyo vilitengwa na serikali kama viwanja vya wazi kwa michezo (open play grounds) na si vya kimkakati wa kujengwa na kuendelezwa. Ndiyo maana katika eneo lisilozidi hekari 20, kulikuwa na viwanja vya timu timu zisizopungua nne. Kwa uchache ni; yanga, simba, cosmo, kongo fc n.k
    Rais wa Simba SC, Evans Aveva anakabiliwa na jukumu la kuifanya SImba SC iwe na Uwanja wake

    Miaka kadhaa ikapita na hatimae wazo la kupata eneo kubwa nje ya mji kwa ajili ya kuanzisha mradi mkubwa wa uwanja wa kimichezo na kibiashara ndipo lilipoibuka na kufanikisha kupata eneo la Bunju. licha ya kuwepo mipango mbalimbali ya uendelezaji wa uwanja Simba eneo hilo la bunju, lakini kwa kuwa hakuna andiko la mradi (project write-up) na hakuna mpango wa matumizi ya ardhi (master plan) mbali na mpango mkakati wa klabu(strategic plan) ulioandaliwa mwaka jana, kutokuwepo kwa maandiko kazi hayo mawili ya mwanzo kumepelekea klabu kwa ujumla kwa maana ya viongozi na wanachama kutokuwa na jibu la moja kwa moja kwamba wapo katika hatua gani ya utekelezaji. Ndiyo maana hata ile tani moja ya saruji iliyochangwa na wanachama wa tawi la wazo haiwezi pimwa kuwa tani hiyo moja ilileta tija gani kunako dhumuni zima la mchango wao la kuchangia ujenzi wa uwanja. Lakini kama andiko mradi lingekuwepo, pengine wanachama hao wangejua au kujilishwa kuwa kwa wakati huo kipaumbele katika mradi huo haikuwa saruji bali labda kuotesha kitalu cha nyasi bora (grass nursery).
    Mengi yamekwisha andikwa juu ya umuhimu wa klabu kujenga na kumiliki uwanja wake( na hili si kwa simba tu na hata yanga), ila kwa kuwa leo lengo langu ni kuijadili simba, ntajikita zaidi kwao.
    nikiwa kama mdau wa michezo, kwa nafasi yangu naomba niwasilishe ushauri wangu kwa klabu ya simba kwa kuzingatia dondoo (highlights) zifuatazo;
    Wataalamu wa masuala ya mipango huongozwa na kauli mbiu kwamba “kupanga ni kuchagua”. Klabu ya simba inajiandaa kupokea takribani nusu bilioni kutokana na kushinda kesi yao FIFA dhidi ya timu ya etoile, basi kuna haja ya kuanza kupanga na kuchagua nini fedha hizo zitafanya kwa manufaa makubwa.(Most feasible benefit margin).
    Binafsi ningepewa  nafasi ya kuulizwa nadhani ni nini fedha hizo zifanywe?haraka kabisa ningesema  ni wakati muafaka kwa klabu hii kutumia fedha hizo kuanza safari ya ujenzi wa uwanja wake wa bunju. Kuna sababu 3 za kitaalamu zinazonishawishi kusema kwamba kama simba haitazitumia fedha hizo katika hili, basi inaweza kuwachukua miaka kadhaa kuendeleza uwanja.
    Sababu 3
    Mosi; malipo ya deni mfu (bad debt). Hii ni lugha ya kihasibu. Maana ya malipo ya deni  mfu, ni lile deni ambalo mtu au taasisi inadai upande wa pili lakini linachelewa sana kulipwa hadi kupoteza kabisa uwezekano wa kulipwa. kiasi cha mdai kujiridhisha kwamba kuendelea kulidai deni hilo ni gharama zaidi kuliko kuliacha. Hivyo mdai huamua kulifuta deni hilo katika vitabu vyake vya mahesabu hususani upande wa mali (assets)au kuliondoa katika mipango yake.
    Inapotokea ghafla mdaiwa anapata uwezo au nguvu ya kisheria kumbana na kisha deni likalipwa, basi mdai hupokea malipo haya kama mapato halisi(pure income). Hivyo basi ‘bad debt’ inapolipwa huhesabika kama chumo la chee kwa sababu moja; kwamba kutokulipwa kwake kusingeathiri mpango uliopo kwa kuwa kiasi hicho kilishaondolewa katika hesabu za mizania za taasisi/kampuni au katika mipango ya taasisi.
    Kwa mantiki hii ndiyo maana nawashauri viongozi wa simba pindi watakapopokea fedha hizo wazihesabu kama ni bad debt iliyokuwa ipo nje ya bajeti yao ya 1.6bil waliyoitangaza awali katika msimu wa ligi hii.wasifanye kosa kuzielekeza ktk matumizi mengine hata kama yawe ni ya muhimu kiasi gani bali waelekeze kwenye mradi wa uwanja.
    Pili; Fedha ya pamoja (lumpsum cash). Deni hili litakapolipwa litaipatia klabu fedha ya mkupuo. Na katika masuala ya uwekezaji inashauriwa kwamba, ili uanzishe mradi mkubwa yakupasa uwe na fedha ya mkupuo mmoja kama kianzio.sababu ya msingi ni kwamba; fedha ya mkupuo mmoja huiwezesha taasisi kupata (acquire) vitu vya msingi (fixed capital) ambavyo havianzi uzalishaji mara moja, ambapo kama ungetumika mkopo kuvianza/kuvigharamia  inaweza pelekea mzigo katika kulipa hususani mradi unapokuwa bado haujakamilika kuanza uzalishaji/kuingiza pato. (own equity has high degree of capital abstinence). Kampuni au taasisi ikiwekeza fedha zake yenyewe katika hizi gharama mgando za awali (fixed cost) huwezesha manufaa ya namna mbili;
    i) Kuwapo na mali za msingi (fixed capital) inayoweza kutumika kupata mkopo (collateral guarantee), au kuwepo kitu kinachoonekana ambacho kinaweza kumvutia mbia mwingine kujiunga katika uwekezaji huo kwa kuuona uwezo hakiki (credibility) ya mtangulizi wake. Na kwa sababu hii ndipo hata ile kampuni ya waturuki mliyowahi kuitafuta sasa mnaweza kuongea lugha moja ya ubia na mkaeleweka  kwa sababu kuna kitu kinaonekana na andiko lipo mkononi lililofanyiwa upembuzi yakinifu wa kiuwekezaji (investment appraisal ) kwa maana pande zote zitaona kuna win-win situation.
    ii) Pindi taasisi ikikopa fedha baada ya gharama hizi za awali kufanywa na taasisi yenyewe, hurahisisha kukishawishi chombo kinachotoa mkopo kwamba, uwezekano wa janga awali (initial investment risk) ni mdogo ambapo uwekezaji mwingi hukwamia hapo. Na kwakuwa upembuzi yakinifu utakuwa umekwisha fanywa na kama utakuwa chanya (viable) hapo mtaona taasisi nyingi za fedha (mortgage financing intermediaries) zitakavyojitokeza kwa kuwa tayari muingie nao ubia wa uwekezaji. Na hasa zile taasisi za mikopo ya muda mrefu. Hii ni kwa sababu; kwa jicho la masuala ya fedha, klabu kama simba inahesabika kwamba ni taasisi itakayokuwepo maisha yote (ever life going concern entity), haitegemei kufa katika karne hii.
    Hivyo basi kutumia fedha hizo kuanzisha mradi huo japo kwa uchache, kunaweza shawishi taasisi nyingine, tofauti na mkienda kuwaonesha vichaka vya bunju vikiwa kama vilivyo sasa. Hapa nasisitiza kuwa, kama karata mmelamba turufu, kitendo cha kupata nusu bilioni kwa mkupuo tena katika mazingira ambayo hamkuitarajia, msichezee fursa hii kwa kuacha kuwekeza katika fixed capital pale bunju.
    Tatu; pato mzalisho (multiplier effect). Katika maarifa ya uchumi kuna dhana inayotoa muongozo juu ya kuchagua aina ya matumizi ya rasilimali iliyopo ili kutoa tija au manufaa zaidi. Dhana hii hujitwa ‘multiplier’ maana yake ni idadi ya mizidisho ambayo uwekezaji Fulani unavyoweza kujinyumbulisha katika kubadilisha kiwango Fulani cha pato. ( a number of times at which a given investment multiplies itself to give the final change in income). Kadiri ambavyo kitako cha uwekezaji  (investment base) kinavyokuwa kipana ndivyo kiwango cha mzidisho wa pato (income) kinaongezeka na pato la mwisho kuwa kubwa.
    Kwa mantiki hii, nawashauri simba tena na tena kwamba fedha hizo zielekezwe katika kuanzisha uwekezaji bunju, ili ziweze kuleta multiplier effect kubwa. Kwani hata kama kuna watu wanadai fedha pengine walikopwa na klabu wakati wa zoezi zima la kumbakiza okwi mwaka juzi, nathubutu kushauri viongozzi wakubali hata kutozwa riba na wadai hao ili wasubiri, na fedha zielekezwe katika uwekezaji pale bunju japo kwa uwanja wa mazoezi, nina uhakika pindi zoezi hilo likikamilika watalipwa tu hata kwa kutumia riba mzidisho ( compound interest) itawezekana. Na bado klabu itabaki na rasilimali achilia mbali mzidisho wa mapato japo mradi utakuwa haujakamilika, pia mapato yatakayopatikana kutokana na kuokoa gharama za kukodi viwanja vya mazoezi, gharama za kukodi gym  achilia mbali mabango na matangazo kwenye matukio kama vile Simba day.
    Mpango wa mradi
    Kwa mujibu wa hali halisi ya soko na iwapo kukafanyika usimamizi wa moja kwa moja wa klabu katika mradi huo (direct supervision ) na kwa kutumia mfumo wa manunuzi wa moja kwa moja  (force account) unaofanywa na mlaji mwenyewe bila kupitia wakala/ dalali, upo uwezekano wa mambo matatu kufanyika;
    1. Kuwekeza katika uwanja wa mazoezi wa nyasi bandia
    2. Kuwekeza katika uwanja wa nyasi za asili
    3. Kuwekeza katika gym na chumba cha mhadhara (lecture theatre)
    Kwa upembuzi wa awali niliofanya, nimebaini kwamba kama simba wakiamua na wakafata taratibu nilizozisema mwanzoni, inaweza kabisa pasi na chembe ya mashaka kupata japo pitch ya nyasi bandia ya hadhi ya kati.
    Nimejaribu kufanya window shopping kupitia mtandao kwa kuitisha nukuu za bei (quotations) toka kampuni mbalimbali zinazotengeneza nyasi bandia za viwanja vya soka (synthetic grass for soccer grounds), nikaona kwamba wastani wa bei ya nyasi bandia zenye kiwango cha ( DTEX 12000, 50mm height , single colour green) bei ni kati ya $ 5 hadi $8 kwa meta moja ya mraba (ninazo nukuu za bei kama rejea). Na kwa mahesabu ya haraka, pitch ina ukubwa wa (100x60)yadi= yadi za mraba 6000. Sasa ili tuende na hesabu kwa haraka kwa vipimo vinavyojulikana na wengi, tuseme yadi za mraba 6000 tuzilinganishe na meta za mraba 6000 (tofauti ni ndogo).
     Hivyo 6000m2 x8$/m2 x Tsh 1740/$= Tsh 83,520,000/= 
    Makadirio ya ushuru (import duty+ excise duty+VAT) na gharama za utoaji mzigo bandarini, jumla haitozidi 50,000,000/= hivyo basi kwa makadirio ya juu, Tsh 150 milioni zinaweza fikisha nyasi bandia bunju. Yapo pia makadirio ya kufanya usawazishaji na uwekaji kokoto kabla ya zuria (levelling and gravelling) pamoja na utandazaji wa zuria. Gharama hizi sitozikadiria moja kwa moja, ila wanaweza itisha nukuu kwa wataalamu wa kufanya kazi ya utandazaji. Ila kwa kutumia mantiki ya ufananisho kazi ili kukadiria gharama (similarity in task assignment), kama shughuli ya kusawazisha na kupanda nyasi za kawaida enzi za mh Rage kulifanywa kwa Tsh 100mil, basi hata tukizidisha mara mbili kwa zoezi la nyasi bandia haitozidi 200mil. Hivyo naamini shughuli zote za zoezi zima la uagizaji na utandazaji wa nyasi bandia itagharimu kiasi kisichozidi 350 mil.
    Uwekezaji mbadala; Uwanja wa nyasi asili endelevu
    Iwapo simba wataamua kufufua uwanja wa nyasi asili lakini kwa muono wa pitch endelevu, napo fedha hizo za mauzo ya okwi zitafanikisha zoezi hilo. Zoezi la kusawazisha na kupanda nyasi, kuanzisha kitalu kidogo cha nyasi za kujazia pindi vipara vinapojitokeza, kuchimba kisima kirefu na kuunganisha pampu na mfumo wa maji kuzunguka uwanja, kushusha transfoma ya umeme uwanjani hapo na mambo mengine madogo madogo, vyote hivyo jumla ya Tsh 200mil zitatosha kabisa. Sambamba na kuajiri mtunza/ watunza uwanja (umwagiliaji na ufidiaji nyasi), hapa kiasi cha Tsh 600,000 hadi 800,000 kinaweza lipwa kwa mwezi kama mishahara.
    Ujenzi wa gym na darasa la mhadhara (kufundishia mbinu)
    Kwa gym ya mazoezi ya viungo yenye mashine mbalimbali 30, itaweza kuhudumia watu 30 kwa mkupuo. Na kwa tathimini ya bei za soko, wastani wa mashine za gym ni kati ya Tsh 800,000 (laki nane) hadi 4,000,000 kulingana na aina ya mashine. Hivyo kwa wastani wa tsh 2,500,000 (milioni mbili na nusu) kwa mashine>,2,500,000x30=75,000,000/= naamini kwa idadi hii ya mashine, itakuwa ni moja ya gym nzuri pengine zaidi ya baadhi ya gym ninazozifahamu. Kwa upande wa darasa la mhadhara lenye uwezo wa kuchukua watu 50, uwekezaji wa Tsh 100milioni naamini kwa wale wanaopajua mlimani watakubaliana nami kwamba kwa kiasi hiki kikitumika vizuri litapatikana darasa zuri kuliko hata lecture theatre za CASS A&B.
    Nihitimishe kwa kusema kwamba, nawaasa viongozi wa klabu ya simba waanze kulijadili suala hili la uendelezaji uwanja mapema, ili watakapolipwa fedha wawe tayari na mpango kazi (action plan) mezani tayari kwa utekelezaji.
    Lakini awali ya yote, nawashauri kabla ya kufanya lolote pale bunju watafute wataalamu wa masuala ya mipango ardhi, ili wawaandalie mpango wa matumizi ya ardhi yao (master plan) kwa mtiririko mzuri.ili pindi utekelezaji ukianza wa jambo lolote lifanyike katika eneo kusudiwa. Mfano wapi uwanja wa timu za vijana uwe, wapi uwanja wa mazoezi uwe, wapi uwanja mkuu wa mechi utakaa, wapi gym,hostel mgahawa n.k vitakaa. Hii itasaidia kuepuka matumizi mabaya ya ardhi pia itaweka mtiririko mzuri (flow) wa shughuli mbalimbali uwanjani hapo.
    Kingine cha muhimu, uongozi ufikirie kuajiri meneja mradi/uwekezaji atakayeratibu shughuli zote za miradi na uwekezaji wa klabu ikiwemo mradi wa uendelezaji uwanja bunju. Huyu asaidie kufanya tathimini za uwekezaji na kuchambua njia za kawaida kabisa (wala si-hisani) za vipi na wapi pa kupata fedha za uwekezaji miradi ya klabu.
    Namaliza kwa kusema, chonde chonde simba, mwanzo wa kuianza safari ya ujenzi wa uwanja wenu ni sasa, msiiache nafasi hii ikawaponyoka. Binafsi ntajitolea kuungana na timu mtakayoiunda kufanya upembuzi wa awali (investment feasibility study) na kuwaandalia (action plan) kwa uwekezaji wa shughuli nilizozijadili hapo mwanzo iwapo mtaona inafaa, ili kuwapa shime kwamba inawezekana.
    Na kwa jinsi wanachama na wapenzi wa klabu yenu walivyonahamu ya kumiliki uwanja wenu, naamini mkianzisha ujenzi hapo mtashangaa hizo tani na tani za saruji na vifaa vya ujenzi, zitakavyo miminika hapo site hadi mtaanza kujiuliza nini kitangulie uwanja au stoo ya kuhifadhi vifaa, kwa jinsi kasi ya wapenzi kujitolea itakavyokuwa kubwa. Na hili likiwezekana kwa simba, hata pale jangwani nataraji tutaona ma greda yanaanza kujaza vifusi kwa kasi ya ajabu. Na huu ndiyo utakuwa mwanzo wa safari halisi wa vilabu vya simba na yanga kujenga viwanja vyao zenyewe na kuachana na nadharia za miaka nenda rudi.
    “Daima kikubwa huanzwa na kidogo ili kupata uzoefu wa kukiendesha kikubwa” huu ni ushauri wangu. Nawasilisha

    (Makala imeandikwa na Hemed HR, Mwanazuoni anayesomea Shahada ya uzamivu (PhD) katika fani ya uchumi, anayebobea eneo la fedha (public finance) Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. 0762955454, sangameydi@yahoo.co.uk)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA NI WAKATI SASA WA KUIANZA SAFARI YA UJENZI WA UWANJA WENU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top