• HABARI MPYA

    Wednesday, October 01, 2014

    NEEMA YAMWAGIKA TASWA, IPTL WAMWAGA MILIONI 20 TUZO ZA WANAMICHEZO BORA TANZANIA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KAMPUNI ya kufua umeme ya IPTL Limited, leo imekabidhi hundi ya Sh. Milioni 20 kwa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) kwa ajili ya tuzo za Wanamichezo Bora nchini, zilizopangwa kufanyika Desemba 12, mwaka huu.
    Akikabidhi hundi hiyo hiyo, Mwenyekiti Mtendaji wa IPTL Limited, Harbinder Singh Sethi katika makao makuu ya kampuni hiyo, Tegeta, Dar es Salaam amesema kwamba ametoa mchango huo kwa sababu anapenda michezo.
    “Nimetoa mchango huu, kwa sababu na mimi napenda michezo, mimi nilikuwa dereva mshindi namba tatu wa mbio za magari Afrika, nawatakia kila heri TASWA wafanikishe zoezi hili, tuko pamoja,” amesema Sethi.
    Mwenyekiti Mtendaji wa IPTL, Harbinder Sing Sethi akimkabidhi mfano wa hundi ya Sh Milioni 20, Mwenyekiti wa TASWA, Juma Pinto kulia

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TASWA, Juma Abbas Pinto amesema kwamba wanashukuru kwa mchango huo wa IPTL, ambao unafungua mfuko wa fedha za kuendeshea zoezi hilo unaohitaji Sh. Milioni 120.
    Katibu wa TASWA, Amir Mhando kwa upande wake amesema maandalizi yanaendelea vizuri na ameomba ushirikiano wa kutosha baina ya waandishi wa habari nchini, ili zoezi hilo lifane.
    IPTL inakuwa kampuni ya pili kuchangia mchakato wa tuzo hizo, baada ya kampuni ya Bakhresa (SSB) Limited kutoka Sh. Milioni 10 wiki iliyopita. 
    Tuzo za wanamichezo bora nchini, mwaka jana zilishindwa kufanyika baada ya waliokuwa wadhamini wake, Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) kujitoa dakika za mwishoni.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NEEMA YAMWAGIKA TASWA, IPTL WAMWAGA MILIONI 20 TUZO ZA WANAMICHEZO BORA TANZANIA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top