• HABARI MPYA

    Friday, October 31, 2014

    MENEJA WA KASEJA ‘ABAMBWA FARAGHA’ NA KIGOGO WA SIMBA SC MBEZI BEACH…NI SIKU MOJA TU BAADA YA KUWACHIMBA MKWARA YANGA SC

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    SIKU moja baada ya kutishia kuvunja mkataba wa mteja wake na klabu ya Yanga SC, Meneja wa kipa Juma Kaseja, Abdulfatah Salim jana amekutwa akizungumza faragha na Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Simba SC, Mohammed Nassor ‘Steven Seagal’.
    Abdulfatah jana alitumia muda wa zaidi ya dakika 30 kuzungumza faragha na Mohamed Nassor, ambaye wengine humuita Mohamed Kigoma baada ya kukutana naye kwenye msiba wa mama wa Zacharia Hans Poppe, eneo la Ununio, Mbezi, Dar es Salaam.
    Mohamed Kigoma alimtangulia Abdulfatah kufika msibani na Meneja huyo wa Kaseja alipoingia kwenye eneo hilo, alikwenda moja kwa moja kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Simba SC.
    Abdulfatah kushoto akizungumza na Mohammed Nassor kulia

    Mohammed alimlaki vizuri kwa furaha Abdulfatah na kuanza kuzungumza naye kwa sauti za chini ili kuzuia watu wengine waliowazunguka kutosikia mazungumzo yao.
    Kama kwamba hiyo haitoshi, wawili hao waliinuka eneo la msibani na kwenda kusimama pembeni kuzungumza kwa muda zaidi ya nusu saa kabla ya kila mmoja kupanda gari lake na kuondoka.
    Juzi, Abdulfatah alisema Kaseja yuko tayari Mkataba wake Yanga SC uvunjwe iwapo klabu hiyo haitatekeleza mambo mawili, moja kuanza kumpa nafasi za kudaka katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Kupitia Meneja wake huyo, Kaseja ameipa masharti Yanga SC kama inataka kubaki naye immalizie dau lake la usajili Sh. Milioni 20 na pia kuanza kumpa nafasi ya kudaka.
    Mohamed Nassor alimpokea kwa furaha Abdulfatah
    Akamkaribisha kiti mbele ya Jerry Yambi

    Kwa sasa, kipa huyo namba moja wa zamani wa Tanzania, hana nafasi kwenye kikosi cha kwanza cha Yanga SC chini ya kocha Mbrazili, Marcio Maximo, tofuti na ilivyokuwa chini ya kocha aliyetangulia, Mholanzi, Hans van der Pluijm alikuwa anadaka kwa zamu na Deo Munishi ‘Dida’.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MENEJA WA KASEJA ‘ABAMBWA FARAGHA’ NA KIGOGO WA SIMBA SC MBEZI BEACH…NI SIKU MOJA TU BAADA YA KUWACHIMBA MKWARA YANGA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top