• HABARI MPYA

    Wednesday, October 29, 2014

    KASEJA AWAPA YANGA SC MASHARTI MAWILI VINGINEVYO MKATABA WAKE ‘UCHANWE CHANWE’

    REKODI YA JUMA KASEJA YANGA SC 

    Yanga SC 3-2 KMKM (Kirafiki, alifungwa mbili Dar)
    Yanga 1-3 Simba SC (Mtani Jembe, alifungwa tatu Dar)
    Yanga SC 0-0 KS Flamurtari Vlore (Ziara ya Uturuki, hakufungwa)
    Yanga SC 3-0 Ankara Sekerspor (Ziara ya Uturuki, hakufungwa)
    Yanga SC 2-2 na Simurq PIK (Ziara ya Uturuki, alifungwa mbili)
    Yanga SC 7-0 Komorozine (Ligi ya Mabingwa, hakufungwa)
    Yanga SC 0-0 Mtibwa Sugar (Ligi Kuu Bara)
    Yanga SC 1-1 Azam FC (Ligi Kuu, alifungwa moja)
    Yanga SC 2-0 Rhino Rangers (Ligi Kuu, hakufungwa)
    Yanga SC 5-0 Prisons (Ligi Kuu)
    Yanga SC 1-2 Mgambo JKT (Ligi Kuu alifungwa mbili)
    Yanga SC 1-0 Chipukizi (kirafiki Pemba, hakufungwa)
    Yanga SC 2-0 KMKM (Kirafiki Zanzibar, hakufungwa)
    Yanga SC 0-0 CDA (Kirafiki Dodoma, hakufungwa)
    Yanga SC 1-0 Ambassador (Kirafiki, hakufungwa)
    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    KIPA Juma Kaseja yuko tayari Mkataba wake Yanga SC uvunjwe iwapo klabu hiyo haitatekeleza mambo mawili, moja kuanza kumpa nafasi za kudaka katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Kupitia Meneja wake, Abdulfatah Salim, Kaseja ameipa masharti Yanga SC kama inataka kubaki naye immalizie dau lake la usajili Sh. Milioni 20 na pia kuanza kumpa nafasi ya kudaka.
    Kwa sasa, kipa huyo namba moja wa zamani wa Tanzania, hana nafasi kwenye kikosi cha kwanza cha Yanga SC chini ya kocha Mbrazili, Marcio Maximo, tofuti na ilivyokuwa chini ya kocha aliyetangulia, Mholanzi, Hans van der Pluijm alikuwa anadaka kwa zamu na Deo Munishi ‘Dida’.
    Abdulfatah ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba, katika Mkataba wao walioingia na Yanga SC, walikubaliana kukamilishia malipo ya mwisho ya dau la usajili ya (Sh Milioni 20) ifikapo Januari 15, mwaka huu, lakini klabu hiyo hadi sasa haijafanya hivyo.
    Amesema wakati wanavumilia hilo, bado mteja wake hana nafasi kwenye kikosi cha kwanza jambo ambalo ni hatari kwa kipaji cha kipa huyo.
    Abdulfatah amesema kwamba wanayaingiza masharti hayo yote kwa maandishi na kuyapeleka kwa uongozi wa Yanga SC uyatekeleze, vinginevyo hatua za kuuvunja mkataba zitafuata. 
    Kaseja anataka kudaka, au kuondoka Yanga 
    Kaseja ameidakia Yanga SC mechi 15 tu tangu amesajiliwa mwishoni mwa mwaka jana, akiwa kipa huru baada ya kuachwa Simba SC, kati ya hizo mechi tano zikiwa za Ligi Kuu na moja ya Ligi ya Mabingwa Afrika.  
    Kwa ujumla katika mechi hizo, Kaseja amefungwa jumla ya mabao 10, yakiwemo matatu Yanga SC ikilala 3-1 mbele ya mahasimu, Simba SC katika mechi ya Nani Mtani Jembe. Mbali na Kaseja na Dida, kipa mwingine Yanga SC ni Ally Mustafa Barthez ambaye ndiye kipa wa tatu katika klabu hiyo yenye maskani yake makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam.
    Makipa wote hao waliwahi kukutana katika klabu ya Simba SC, mahasimu wakubwa wa Yanga SC na Kaseja alikuwa kipa chaguo la kwanza mbele ya makocha tofauti dhidi ya wenzake hao timu hiyo ya Msimbazi.
    Pamoja na kuwa kipa chaguo la kwanza Simba SC, Kaseja hakuwahi kumvutia kocha Maximo alipokuwa akiifundisha timu ya taifa, Taifa Stars na wakati fulani alidiriki kuwaita Barthez na Dida kudakia timu ya nchi, akimuacha Juma.
    Meneja amecharuka; Abdulfatah Salim anataka Kaseja adake Yanga SC, au mkataba uvunjwe
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KASEJA AWAPA YANGA SC MASHARTI MAWILI VINGINEVYO MKATABA WAKE ‘UCHANWE CHANWE’ Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top