• HABARI MPYA

    Friday, October 24, 2014

    HUSSEIN SHARRIF ‘CASILLAS’: MCHEZAJI WA ORLANDO ALINIKANYAGA KWA KIATU CHA CHUMA NA KUNICHANA VIBAYA UGOKO

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MLINDA mlango wa pili wa Simba SC, Hussein Sharrif ‘Casillas’ amesema kwamba aligongwa kwa kiatu chenye ‘njumu’ za chuma na mchezaji wa Orlando Pirates ya Afrika Kusini na kuchika vibaya ugoko wake.
    Casillas alitolewa mwishoni mwa kipindi cha kwanza Oktoba 11, mwaka huu akiidakia Simba SC katika mchezo wa kirafiki uliomalizika kwa sare ya bila kufungana baada ya kuumia, nafasi yake ikichukuliwa na kipa wa tatu, Peter Manyika.
    “Niliruka vizuri tu, mguu ukiwa juu ili kujikinga, sasa jamaa akaja kunikanyaga kwenye mguu uliokuwa chini na sikuwa na namna ya kuutoa kwa sababu tayari mguu mmoja ulikuwa juu. Niliumia sana,” anasema Casillas katika mahojiano na BIN ZUBEIRY jana Kigamboni, Dar es Salaam.
    Casillas akisaidiwa na mkewe kujivuta kwa magongo nyumbani kwake, Mji mwema, Kigamboni, Dar es Salaam
    Hii ndiyo sehemu ya goti aliyopasuliwa Casillas ili kuunganishwa ugoko uliochanika

    Hata hivyo, Casillas anasema anashukuru baada tu ya kuumia alipelekwa katika hospitali ya Netcare Milpark mjini Johannesburg, ambako alipatiwa tiba nzuri. 
    Casillas aliumia wakati Simba SC imeweka kambi ya wiki moja na ushei Afrika Kusini kujiandaa na mchezo dhidi ya mahasimu wao, Yanga SC uliofanyika Oktoba 18, mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    “Niseme tu nashukuru haya yalitokea nikiwa Afrika Kusini nikapatiwa tiba nzuri, sijui kama ingetokea nikiwa hapa (Dar es Salaam) ingekuwaje, yaani namshukuru sana Mungu,”anasema.
    Casillas anasema alifanyiwa upasuaji wa kiwango cha juu, kuungwa ugoko wake uliopasuka na baadaye kushonwa kwa nyuzi ngumu mfano wa waya.
    Anasema baada ya tiba hiyo akatakiwa kupumzika kwa wiki sita kabla ya kuanza mazoezi mepesi na kwamba anatarajia hadi kufika Desemba atakuwa fiti kabisa kurejea uwanjani.
    Casillas ambaye atafungua nyuzi alizoshonwa baada ya wiki tatu, anasema anasikitika aliumia katika kipindi ambacho tayari kipa wa kwanza wa timu yao, Ivo Mapunda alikuwa majeruhi naye.
    “Timu ilikuwa katika wakati mgumu, siyo kwa sababu tu ilibaki na kipa wa tatu bwana mdogo, hapana, bali pia ilibaki na kipa mmoja tu na tulikuwa tunaelekea katika mchezo mgumu dhidi ya Yanga SC,”. 
    “Lakini nashukuru sana, dogo amedaka vizuri ile mechi hakufungwa na timu imetoa sare. Na ninamuombea sana Peter aendelee vizuri katika kipindi hiki ambacho mimi ni brother (kaka) Ivo hatupo,”anasema mume huyo wa Husna, waliyezaa naye mtoto, Abubakar mwenye umri wa miezi sita sasa. 
    Casillas akiwa na tuzo zake za kipa bora wa SPUTANZA kulia na Ligi Kuu kushoto
    Casillas akiwa na mwanawe Abubakar nyumbani kwake Mji Mwema 

    Mkazi huyo wa Mji Mwemba, Kigamboni, Dar es Salaam anasema kwamba bado hajaweza kuanza kutembea kwa sasa, akiwa anatumia magongo kutembea umbali mfupi- tena inapobidi, kwani anashinda nyumbani kwake tu kwa sasa akijiuguza.
    “Ninamshukuru sana mke wangu Husna, ni mke mwema, yuko nami katika wakati huu mgumu na ananisaidia sana kwa kweli, napata faraja,”anasema.
    Casillas amesajiliwa Simba SC msimu huu akitokea 
    Mtibwa Sugar ya Morogoro aliyoanza kuichezea mwaka 2010 akitokea Villa Squad ya Dar es Salaam.
    “Nilijiunga na Mtibwa baada ya kuipandisha Villa Squad Ligi Kuu na nikawa na bahati ya kuingia Mtibwa na moja kwa moja kuwa kipa wa kwanza, kwa sababu ndiyo msimu ambao Kado (Shaaban) alikuwa amekwenda Yanga SC (sasa yupo Coastal Union),”anasema.
    Kipa huyo bora wa Ligi Kuu msimu uliopita, alizaliwa Juni 3, mwaka 1994 Mbagala mjini Dar es Salaam na alisoma katika shule mbili za Msingi, kwanza Kizuiani hadi darasa la sita na baadaye Kibasila, ambako alikwenda kurudia darasa la tano. 
    Alipomaliza elimu ya Msingi, akajiunga na Sekondari ya Kibasila, ambako hata hivyo safari yake ya kimasomo iliishia kidato cha Pili, kutokana na kutekwa zaidi na soka. 
    Fahari FC ndiyo timu ya kwanza ya ushindani kuchezea Casillas akiwa na wachezaji wengine walioibuka nyota baadaye nchini kama Julius Mrope kabla ya kuhamia Phanton Power, zote za Tandika ambako alikuwa na Said Mkopi waliyekutana pia Mtibwa baadaye. 
    Baadaye Basillas akahamia Mkunguni FC ya Ilala kabla ya kujiunga na Villa Squad, ambayo ilimfanya aonekane Mtibwa Sugar na sasa yupo Simba SC.
    Casillas alirejea anasukumwa kwenye kiti cha walemavu kutoka Afrika Kusini

    Mwaka 2010 Casiilas aliitwa timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 20, Ngorongoro Heroes kabla ya kupandishwa U23 na baadaye timu ya wakubwa mwaka 2012 chini ya kocha Kim Poulnse kutoka Denmark.
    Kabla ya kutwaa tuzo ya kipa bora wa Ligi Kuu msimu uliopita, Casillas pia alishinda tuzo ya kipa bora wa Chama cha Wachezaji Tanzania (SPUTANZA) mwaka jana.
    “Kupata tuzo ni jambo zuri la kujivunia, inaonyesha kazi yako imekubalika, nilifurahi sana. Lakini ndoto yangu ni kushinda mataji na Simba SC na tuzo zaidi,”anasema.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HUSSEIN SHARRIF ‘CASILLAS’: MCHEZAJI WA ORLANDO ALINIKANYAGA KWA KIATU CHA CHUMA NA KUNICHANA VIBAYA UGOKO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top