• HABARI MPYA

    Wednesday, October 01, 2014

    AISHI MANULA NA MWADINI ALI KAMA NEMES NA MWAMEJA AU RIFFAT SAID ENZI ZAO

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KIKOSI cha timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, kitakachomenyana na Benin katika mechi ya Kalenda ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) Oktoba 12 mwaka huu mjini Dar es Salaam kimetajwa.
    Kocha Mholanzi Mart Nooij ameteua wachezaji 26, wakiwemo makipa wawili wa Azam FC, Aishi Manula na Mwadini Ali. 
    Unaweza kujiuliza, inakuwaje Nooij anaita makipa wawili kutoka klabu moja, wakati Ligi Kuu pekee ina klabu 14- maana yake kuna makipa wengine 13 wanasimama kwenye milingoti.
    Makipa wa Azam FC, Aishi Manula kushoto na Mwadini Ali kulia wakijiandaa kabla ya mechi ya klabu yao

    Kutoka klabu nyingine 13, Nooij amechukua kipa mmoja, Deogratius Munishi ‘Dida’ ambaye kwa sasa ndiye ‘Tanzania One’.
    Masuala ya kiufundi hayo anaachiwa mwalimu mwenyewe- lakini kitu kinachoonekana ni namna makipa hao wanavyoishi vizuri na makocha wa Azam FC, chini ya Mcameroon, Joseph Marius Omog wanavyoweza kulinda vipaji vyao kwa kuwapa nafasi kwa awamu.
    Wote bora, na pale Azam FC wanadaka kwa kupokezana, huu ukiwa msimu wa pili sasa, yaani hiyo ni tangu enzi za kocha Muingereza Stewart Hall.
    Maisha ya makipa hayo, yanakumbusha enzi zile klabu moja walipokutana makipa bora hadi watatu na wakadaka kwa kupokezana na wakati mwingine wote kuitwa timu ya taifa.
    Kuna wakati Simba SC ilikuwa ina Mwameja Mohamed, Steven Nemes na Joseph Katuba (marehemu) na wote walikuwa wanaitwa Taifa Stars na kudaka kwa awamu.
    Kuna wakati Yanga SC waligongana Nemes na Riffat Said (marehemu) na wote walikuwa wanaitwa Taifa Stars na kudaka kwa awamu.
    Kikosi cha Simba mwaka 1993 makipa Mwameja Mohamed na Joseph Katuba walikuwa wakiitwa pamoja Taifa Stars

    Kwa hivyo hata Aishi Manula na Mwadini kuwa pamoja Azam FC na kuitwa wote Taifa Stars si jambo geni. 
    Ni kitu ambacho hata kesho kocha wa Yanga SC, Mbrazil, Marcio Maximo akiamua anaweza kuanza kumpanga na kipa mwingine kati ya wengine wawili wazoefu alionao Juma Kaseja na Ally Mustafa ‘Barthez’ na akionyesha uwezo pia, naye anaweza kuungana na Dida kuitwa Stars.
    Hata Patrick Phiri wa Simba SC naye anaweza kuamua kutosubiri hadi kipa mmoja aumie ili kumpanga mwingine, kwa kuwapa nafasi kwa zamu makipa wake watatu bora, Ivo Mapunda, Hussein Sharriff ‘Cassilas’ na Peter Manyika.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AISHI MANULA NA MWADINI ALI KAMA NEMES NA MWAMEJA AU RIFFAT SAID ENZI ZAO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top