• HABARI MPYA

    Tuesday, September 02, 2014

    SIMBA SC KUCHEZA NA GOR MAHIA JUMAMOSI TAIFA, BADA YA HAPO APR

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC inarejea Dar es Salaam Ijumaa na Jumamosi itacheza mchezo wa kirafiki dhidi ya Gor Mahia ya Kenya Uwanja wa Taifa, kisha kupanda boti kurejea visiwani Zanzibar. 
    Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Simba SC, Mohammed Nassor ‘Steven Seagal’ ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba maandalizi ya mchezo wa Jumamosi yanaendelea vizuri.
    Amesema baada ya mchezo huo, kikosi kitarejea Zanzibar kuendelea na kambi yake ya kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Mafundi wa mpira; Viungo wa Simba SC, Amri Kiemba kulia na Shaaban Kisiga kushoto 

    Hata hivyo, kuna uwezekano Simba SC ikarejea Dar es Salaam wiki ijayo, kwa ajili ya mchezo mwingine wa kirafiki dhidi ya washindi wa pili Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, APR ya Rwanda.
    Mchezo huo umepangwa kufanyika Uwanja wa Taifa pia, Jumatano ijayo baada ya timu hiyo ya Kigali kucheza na Yanga SC Jumapili hii kwenye Uwanja huo huo uliopo Temeke, Dar es Salaam.
    Mfululizo wa mechi za kirafiki Uwanja wa Taifa, unaanza kesho kwa mchezo kati ya Thika United ya Kenya na Yanga SC.
    Ligi Kuu inatarajiwa kuanza Septemba 20, mwaka huu, mabingwa watetezi Azam FC wakianza na Polisi Morogoro Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam Septemba 20, mwaka huu, wakati Yanga SC waliomaliza nafasi ya pili wataanza na Mtibwa Sugar Uwanja wa Jamhuri, Morogoro siku hiyo.
    Washindi wa tatu, Mbeya City wataanza na JKT Ruvu ya Pwani, Uwanja wa Sokoine, Mbeya Septemba 20 na washindi wa nne, Simba SC wataanza na Coastal Union ya Tanga Septemba 21, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Mechi nyingine za ufunguzi za Ligi Kuu zitakuwa kati ya Stand United watakaoikaribisha Ndanda ya Mtwara Uwanja wa Kambarage, Shinyanga, Mgambo JKT wataikaribisha Kagera Sugar Uwanja wa Mkwakwani, Tanga na Ruvu Shooting watakuwa wenyeji wa Prisons Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC KUCHEZA NA GOR MAHIA JUMAMOSI TAIFA, BADA YA HAPO APR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top